Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Kiongozi wa upinzani Zambia Hichilema aachiliwa huru

MTEULE THE BEST
Sambia Hakainde Hichilema (Getty Images/AFP/D. Salim)
Kiongozi wa upinzani nchini Zambia, wa chama cha UPND, Hakainde Hichilema aliachiliwa huru Jumatano baada ya kiongozi wa mashtaka nchini humo Bibi Lillian Siyunyi kuyaondoa mashitaka ya uhaini dhidi yake.

Mahakama kuu nchini Zambia imefutilia mbali kesi ya uhaini dhidi ya kiongozi wa upinzani nchini humo Hakainde Hichilema na kumuachilia huru na wenzake watano. Hii ni baada ya kiongozi wa mashtaka kuyaondoa mashtaka dhidi ya Hichilema bila ya kutoa sababu maalum.
Kiongozi wa upinzani wa chama cha Umoja kwa Maendeleo ya Kitaifa nchini Zambia, UPND, Hakainde Hichilema aliachiliwa huru leo baada ya kiongozi wa mashtaka nchini humo Bibi Lillian Siyunyi kuiambia mahakama ya Lusaka kuwa anaondoa mashitaka dhidi ya Hichilema pamoja na maafisa wengine watano wa chama chake ambao wote walikanusha tuhuma za uhaini dhidi yao. Upande wa mashtaka haukutoa sababu za kuyaondoa mashtaka hayo.
Rais wa Zambia Edgar Lungu
Rais wa Zambia Edgar Lungu
Hofu ya kukamatwa kwake tena
Msemaji rasmi wa chama cha upinzani cha National Restoration Party, Narep Bwalya Nondo, amesifia kuachiliwa huru kwa Hichilema, lakini angali anahofu kuwa Hichilema angali anaweza kupokonywa uhuru wake.
"Tunayofuraha kuwa mwenzetu ameachiliwa kutoka jela, lakini tunahuzunika kuwa hana uhuru kwa sababu wasilisho la serikali mahakamani halimruhusu mshukiwa yeyote wa uhalifu kuwa na uhuru kamili, anaweza kukamatwa tena kwa mashtaka hayohayo na arudishwe mahakamani. Ndiyo sababu tunataka serikali kufutilia mbali kesi hiyo kwa manufaa ya Amani na upatanisho wa dhati ili taifa lifungue ukurasa mpya."
Alizuia msafara wa rais Lungu
Afisa wa polisi mbele ya wafuasi wa Rais Lungu katika kampeni za mwaka 2016
Afisa wa polisi mbele ya wafuasi wa Rais Lungu katika kampeni za mwaka 2016
Hichilema alikamatwa mwezi Aprili mwaka huu na kushtakiwa kwa uhaini kufuatia kisa cha msafara wake kutouachilia njia msafara wa Rais Edgar Lungu na akalaumiwa kwa kuhatarisha maisha ya rais kwa lengo la kuchukua mamlaka.
Kesi hiyo ya uhaini ilikuja baada ya Hichilema kushindana na Rais Lungu katika uchaguzi wa urais mwaka uliopita ambapo Lungu alitangazwa mshindi kwa asilimia 50 ya kura dhidi ya 47 ya Hichilema.
Baadaye Hichilema aliwasilisha kesi ya kupinga ushindi wa Lungu mahakamani. Baadhi ya wafuasi wake walijitokeza nje ya mahakama kuelezea furaha yao. Patricia Banji ambaye ni mwenyekiti wa jinsia katika chama cha UPND ni mmoja wao.
"Ninayo furaha hata naweza kuongea sana kw akuona rais wetu na hili ndilo tumekuwa tukisubiri kwa muda mrefu. Tulijua siku moja rais wetu ataachiliwa huru. Leo Zambia na dunia kwa jumla inafuraha kwa kumuona rais wetu yuko huru."
Wito wa wafungwa wa kisiasa kuachiliwa huru
Afisa wa uchaguzi wa Zambia akibeba karatasi ya kura
Afisa wa uchaguzi wa Zambia akibeba karatasi ya kura
Muda mchache baada ya kuachiliwa kwake, mwenyewe Hichilema aliitolea wito kuwaachia huru wafungwa wengine wote wa kisiasa walioko magerezani.
Kwa miaka mingi, taifa hilo la Afrika Kusini limeshuhudia upokezanaji wa mamlaka kwa njia ya amani na hata kusifiwa na Umoja wa Mataifa kama mfano bora kwa Afrika. Lakini katika uchaguzi uliopita, kulitokea ghasia za kisiasa.
Makundi ya kutetea haki za kibinadamu yalitaja kesi dhidi ya Hichilema kama hatua ya kunyamazisha sauti za wapinzani
Zambia imekuwa katika hali ya tahadhari tangu mwezi Julai mwaka huu kufuatia ghasia na taharuki zilizoshuhudiwa. Hali hiyo ya tahadhari inatarajiwa kudumu hadi mwezi Oktoba. Rais Lungu ametaja vurugu hizo kuwa njama za kuvuruga uchumi wa nchi.
Mwandishi: John Juma/ APAE/DPAE
Mhariri: Mohammed Khelef

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

MAPENZI: Kuna faida na ni muhimu Mpenzi wako kuwa rafiki yako pia

Kuna faida kubwa kwa wapenzi kuwa marafiki KUTOKANA na mila mbalimbali, baadhi ya watu wamekuwa wakiamini kwamba mwanamke ni daraja la pili. Daraja la kwanza na lenye kuthaminiwa ni mwanaume. Yaani mwanamke hana kauli kwa mwanaume. Anakuwa kama mtumwa fulani hivi.  Mwanaume akiongea, basi ni maelekezo kama vile rais wa nchi anavyotoa maelekezo kwa watu walio chini yake. Hakuna wa kupinga. Akisema sitaki kitu fulani kifanyike, basi ni mpaka atakapotoa maelekezo mengine. Vinginevyo, maelekezo ya awali yatabaki kusimama kama sheria.  Wapo baadhi ya wanawake wanaofurahia aina hii ya uhusiano kwa sababu ya mazoea. Kwamba wamekuzwa hivyo, mwanaume ni mwanaume. Huu ni mfumo ambao watu wengi wamekuwa wakiuishi. Kuna ambao wanakubaliana nao, wengine hawakubaliani nao.  Watu wengi sana wamekuwa wakiishi katika malumbano katika mahusiano yao kutokana na mfumo huu wa maisha. Mwanamke hataki kuishi kama mtumwa, mume anakomaa kuonesha uanaume wake. Hakuna anayekubali kushuka,...

Urusi: Vikwazo dhidi ya Korea Kaskazini havitafua dafu

MTEULE THE BEST Image caption Waziri wa maswala ya kigeni nchini Urusi Sergei Lavrov na mwenzeka wa Marekani Rex Tillerson Waziri wa maswala ya kigeni nchini Urusi Segei Lavrov amemwambia waziri wa ulinzi nchini Marekani Rex Tillerson kwamba kuiwekea vikwazo zaidi Korea Kaskazini hakutafua dafu. Taarifa iliochapishwa na wizara ya kigeni nchini Urusi inasema kuwa wawili hao walizungumza kwa njia ya simu na kushutumu majaribio ya makombora ya hivi karibuni yaliotekelezwa na Pyongyang . Lakini inasema kuwa bwana Lavrov alisisitiza kwamba diplomasia ndio njia ya pekee ya kumaliza wasiwasi katika rasi ya Korea, na kutaka hatua zozote dhidi ya taifa hilo kusitishwa akionya huenda zikasababisha madhara yasiojulikana. Waziri wa ulinzi nchini Marekani amesisitiza kuwa bado kuna fursa ya kidiplomasia katika kukabiliana na Korea Kaskazini. Mapema rais Trump alichapisha ujumbe katika akaunti yake ya Twitter akisema mazungumzo sio suluhisho.

Fuvu la binadamu wa kale liligunduliwa miaka 60 iliyopita nchini Tanzania

Fuvu la binadamu wa kale liligunduliwa miaka 60 iliyopita nchini Tanzania Miaka 60 siku kama ya leo ugunduzi mkubwa ulifanyika katika eneo la Olduvai Gorge, kwenye kreta ya Ngorongoro. Wanaakiolojia Louis na Mary Leakey waligundua fuvu la mtu anayeaminika kuwa ni wa kale zaidi waliyompa jina la Zinjanthropus. Ugunduzi huo uliofanyika saa nne asubuhi Julai 22, 1959 kipindi hicho kwenye eneo la Tanganyika ulikuwa wa vipande zaidi ya 100 ukasaidia katika kutambua asili ya watu wa awali duniani. Kabla ya ugunduzi huo, wanasayansi na wanahistoria walikuwa wakiamini kuwa binadamu wa kale walitokea Uchina baada ya ugunduzi wa mafuvu ya kale baina ya 1923 na 1927 nchini humo ya Homo eractus, ama maarufu kama Peking Man. Mafuvu hayo ya Uchina yalikuwa na umri wa takribani miaka 750,000. Mafuvu ya Olduvai eneo ambalo kwa sasa lipo Tanzania wakati wa ugunduzi wake lilikuwa na umri wa takribani miaka milioni 1.75, na hakuna mabaki ya mtu wa kale zaidi ambayo mpaka sasa yamegundul...