Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza limefanikiwa kumuokota mtoto mmoja wa kike akiwa hai anayekadiriwa kuwa na umri wa siku 2 hadi 3 baada ya kutupwa kichakani kandokando mwa ziwa Victoria na mtu asiyefahamika maeneo ya Bwiru ziwani Wilayani Ilemela.
Tukio hilo limetokea Novemba 1, 2018 hii ni baada ya watu waliokua wakipita njiani kusikia sauti ya mtoto akilia toka kichakani ndipo walifuatilia na walipoona ni mtoto walitoa taatifa Polisi.
Polisi walifanya ufuatiliaji wa haraka hadi eneo la tukio na kukuta mtoto wa kike akiwa ametupwa kichakani hapo akiwa hai huku mwili wake ukiwa umeviringishwa kwenye mfuko wa sandarusi.
Jeshi la Polisi limeeleza kuwa Mtoto huyo amepata matibabu na hali yake inaendelea vizuri amekabidhiwa katika shirika la Forever Angel lililopo Bwiru Wilayani Ilemela kwa ajili ya hifadhi.
Hata hivyo Jeshi la Polisi linaendelea na upelelezi pamoja na msako mkali wa kumtafuta mama wa mtoto huyo
Maoni